Tuesday, 31 January 2017

WATU 6 WAUAWA MSIKITINI CANADA KATIKA SWALA YA ISHA'A

Watu sita wameuawa na wengine wanane kujeruhiwa wakati watu wenye silaha waliposhambulia msikiti mjini Quebec juzi baada ya swala ya ya Isha'a, ambapo waziri mkuu wa Canada Justin Trudeau aliliita shambulio hilo kuwa ni la kigaidi. 
Polisi wamesema watuhumiwa wawili wamekamatwa, lakini hawakutoa maelezo zaidi, ama kitu gani kimesababisha kufanya shambulio hilo. 
Hapo mapema Imamu wa msikiti huo alisema watu watano wameuawa na watu walioshuhudia walisema hadi watu watatu waliokuwa na silaha walifyatua risasi dhidi ya watu karibu 40 waliokuwa katika msikiti huo ndani ya kituo cha utamaduni cha waislamu mjini Quebec.
Waziri mkuu Justin Trudeau alisema katika taarifa kwamba anashutumu shambulio hilo la kigaidi dhidi ya Waislamu katika kituo hicho cha ibada. 

Wakati huo huo rais wa Ufaransa Francois Hollande ameshutumu shambulio hilo akisema ni msimamo wa amani na uwazi wa watu wa Quebec ambao magaidi walitaka kushambulia.
Kituo hicho cha Kiutamaduni cha Kiislamu mjini Quebec kimekuwa kikilengwa na watu wenye  chuki dhidi ya Uislamu mara kwa mara. 

Mwezi Juni mwaka jana wakati wa Ramadhani, watu wenye chuki dhidi ya Uislamu waliweka kichwa cha nguruwe katika mlango wa msikiti huo.