Wanandoa Waislamu wamelituhumu Shirika la Ndege la Marekani la Delta Airlines kwa kuwa na chuki dhidi ya Uislamu baada ya kuwazuia kusafiri na ndege ya shirika hilo mjini Paris.
Wahudumu wa ndege hiyo waliwazuia kusafiri na ndege hiyo hivi karibuini kutokana na kile kilichodaiwa kuwa ‘walikuwa wakitokwa na jasho’ huku wakitamka neno Allah, madai ambayo wawili hao wamekanusha.
Faisal Ali na Nazia Ali walikuwa tayari wameshaingia ndani ya ndege ya Delta Airlines na kukaa kwa muda wa dakika 45 wakisuburi kuondoka Paris, Ufaransa kurejea Cincinnati, Ohio Marekani, wakati mfanyakazi wa Delta alipowaamuru wanandoa hao kuondoka nje ya ndege kwa kuwa alitaka kuwauliza maswali.
Aidha walitakiwa kubeba mizigo yao kwani ilikuwa imeshaamuliwa kuwa hawatasafiri kwa ndege hiyo, Bi. Ali alisema walishtushwa sana na kitendo hicho.
Walipohojiwa na polisi mjini Paris walisema walikuwa mjini humo kusherehekea mwaka wa 10 wa ndoa yao na hapo maafisa wa polisi wakasema wamebaini kuwa hawana kosa.
Bw. Ali amesema yamkini alitokwa na jasho kutokana na hali mbaya ya mzunguko wa hewa ndani ya ndege kwani walikuwa wameshasubiri dakika 45 pasina na ndege kuondoka.
Baada ya kuruhusiwa kusafiri siku iliyofuata, wawili hao wanasema walisailiwa tena walipowasili Marekani.
Wanasema vitendo hivyo vya kuwazuia kusafiri na kuwasaili ni udhalilishaji mkubwa.
Baraza la Mahusiano ya Uislamu na Marekani CAIR, ambalo hutetea maslahi ya Waislamu nchini humo, limesema limewasilisha lalamiko dhidi ya shirika hilo la ndege kutokana na kubaguliwa wanandoa hao.
Wakili wa CAIR, Sana Hassan amesema Bwana na Bi Ali, ambao wana asili ya Pakistan, walilengwa kutokana na kuonekana kuwa ni Waislamu.
